Na. WMJJWM, Dodoma
Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt John Jingu amewataka watumishi kuzingatia maadili ya kazi ikiwa ni pamoja na kutunza siri za utumishi wa umma katika utekelezaji wa majukumu yao.
Dkt. Jingu ameyasema hayo Juni 6, 2025, Jijini Dodoma wakati akizungumza na watumishi wapya waliopangwa kufanya kazi katika Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.
"Niwapongeze kwa kuaminiwa na kupata nafasi hii adhimu, nendeni mkafanye kazi kwa bidii huku mkizingatia maadili ya utumishi wa Umma, kafuateni sheria na taratibu zilizowekwa ambazo zinaelekeza nini kifanyike na nini kisifanyike.” amesema Dkt Jingu.
Aidha Dkt Jingu ameongeza kuwa watumishi hao wanapaswa kuzingatia usiri wa taarifa za umma huku akisisitiza kuwa milango ya ofisi yake iko wazi kwa wote wenye mawazo ya kuboresha utendeji kazi ili kufikisha uduma bora kwa jamii.
Sanjari na hayo ameongeza kuwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu imeweka mazingira wezeshi kwa watumishi wa umma ikiwemo fursa zinazotolewa na taasisi za fedha na amewasihi watumishi hao kuzitumia.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake Afisa Ustawi wa Jamii Msaidizi Caroline Emili amesema kuwa wanajivunia kuwa sehemu ya watumishi wa Wizara hiyo na kuahidi kufanya kazi kwa bidii, ubora, weredi na nidhamu. Ikiwemo kuitumia vyema taaluma yao katika jamii.
Wizara imepokea watumishi wapya 39 wakiwemo Maafisa Ustawi wa Jamii Wasaidizi 25, Mafundi Sanifu wawili, Wahudumu wa Afya wanne, Wapishi wawili, Waandishi waendesha Ofisi watatu, Afisa Hesabu Msaidizi mmoja, Afisa TEHAMA mmoja na Afisa Muuguzi mmoja.