Kamishna wa Huduma za Urekebu wa Jeshi la Magereza, CP Amina Kavirondo, akimuwakilisha Mkuu wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Yoram Katungu, alishiriki katika ujumbe wa Tanzania uliohudhuria Mkutano wa 28 wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), uliohitimishwa Julai 18, 2026, mjini Salima, Malawi.
Ushiriki wa Kamishna wa Huduma za Urekebu katika mkutano huo unaonesha mchango wa Jeshi la Magereza katika masuala ya usalama wa Taifa na ushirikiano wa kikanda, sambamba na dhamira ya Tanzania ya kuimarisha amani, ulinzi na usalama ndani ya nchi na katika ukanda wa SADC.
Tanzania, ikiwa ni miongoni mwa nchi waasisi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ilishiriki kikamilifu katika Mkutano huo ambao ulianza kwa vikao vya ngazi ya Makatibu Wakuu vilivyofanyika Julai 13 na 14, 2026, na kufuatiwa na vikao vya ngazi ya Mawaziri vilivyofanyika Julai 16 na 17, 2026.
Katika ngazi ya Mawaziri, ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. James Millya, aliambatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Ayoub Mohammed Mahmoud. Aidha, katika ngazi ya Makatibu Wakuu, Tanzania iliwakilishwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Said Shaib Mussa, pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Dkt. Maduhu Kazi.
Mkutano huo ulisisitiza umuhimu wa utekelezaji wa maazimio yaliyofikiwa na nchi wanachama ili kuendelea kuimarisha amani, ulinzi na usalama katika ukanda wa SADC, kwa kutambua kuwa mazingira ya amani na utulivu ndiyo msingi wa maendeleo endelevu ya wananchi wa ukanda huo.



